Archive for September 18th, 2012
Kigogo … hadi Dar es Salaam
Ni jinsi jiji la Dar linavyoonekana kutokea mzunguko wa barabarani wa Kigogo. Jiji linajongea kwa kasi kubwa. Ukizingatia kwamba kuna barabara ya kukatisha Jangwani inayojengwa kwa kiwango cha lami … Ile nunua nunua ya majengo na viwanja iliyokuwa Kariakoo miaka michache iliyopita bila shaka itahamia Kigogo na maeneo mengine ya jirani.
Hii ina maana kwamba wakaazi wa Kigogo, hasa wanaomiliki majengo na viwanja, wajiandae na vishawishi vya kununuliwa. Ni vema kujifunza kutokana na makosa yaliyofanywa na baadhi ya wazawa wa Kariakoo. Wachukue upande ule mzuri wa mafunzo kutokana na baadhi nyingine ya watu wa Kariakoo. Ni muhimu kulinda ardhi na kutoiuza kiholela kwa kiasi cha fedha ambacho baada ya miaka mitatu kinakuwa kimeyeyuka. Ni afadhali sana kuingia kwenye biashara ya ubia ili kwamba wenye kiwanja na vizazi vyao waendelee kunufaika miaka nenda, miaka rudi.
Ni muhimu kwa wakazi wa Kigogo kujiandaa kwa mabadiliko yanayowanyemelea kwa kasi. Pamoja sana!
Ajali … Kinyerezi
Ni ya uso kwa uso … Hiace na Lorry
Viti vya kwenye Hiace … viliparaganyika na vingine kung’oka
Mparaganyiko wa viti kwenye daladala …
Barabara ilifungwa kwa muda … kisha magari yalianza kupita upande mmoja wa barabara kwa kusubiriana
Ni majira ya saa 2 usiku. Wakati ninawasili eneo la tukio, kiasi cha kama dakika kumi zilikwishapita. Ni basi dogo, Hiace, na lorry la kama tani tatu yaliyohusika na ajali hii. Magari haya kwa yanavyoonekana, yaligongana uso kwa uso. Baada ya kutazama, inaelekea kwamba dereva wa lorry ndiye aliyehama kutoka upande wake wa barabara na hatimaye kugongana na daladala hilo. Baadhi ya abiria waliokuwa kwenye daladala hilo bado wapo. Wengine bado wana mshtuko wa kuhusika kwenye ajali. Wananieleza kwamba walioumia hasa ni madereva wote wawili wa magari hayo. Madereva hao hawapo hapo lakini wamekwishatoka, hakuna aliyejua hasa wako wapi. Lorry lilikuwa likiteremka kwenye kilima kutoka upande wa Kinyerezi na Haice ilikuwa ikipanda kilima hicho kutoka Njia Panda Segerea.
Ajali. Barabara ni nyembamba na ina miteremko mikali kidogo na madaraja daraja. Ingawa hakuna aliyepoteza maisha katika tukio hili, lakini mtu unapata maswali mengi. Linaloumiza kichwa zaidi ni kuhusu umahiri wa madereva wetu hapa nchini. Ajali zilizo nyingi zinasababishwa na uzembe wa madereva. Mtu unajiuliza, hivi hizi leseni zilizo mikononi mwa madereva … wanazistahili kweli? Je, vigezo vyote na masharti yalizingatiwa kabla ya kuwapa leseni hizo? Je, polisi wa usalama barabarani wanafanya kazi yao kikamilifu … au ndiyo baadhi wanawalinda wahalifu wa makosa ya barabarani baada ya kulambishwa shilingi mbili tatu?
Tupige vita ajali. Tunaweza kuwa na barabara zilizo salama katika nchi yetu. Kila mmoja atimize wajibu wake vizuri. Pamoja sana!