Ukwepaji Kodi … Nchi Changa Zayakabili Makampuni ya Kimataifa

Wafanyakazi katika mgodi. Je, kuna uwiano wa kimapato kati ya kinachozalishwa katika migodi na kinachoingia katika mikono ya serikali kupitia kodi? Nchi nyingine zinazoendelea zinachukua hatua zipi? Soma habari hii.
Ukwepaji Kodi: Nchi Zinazoendelea Zayakabili Makampuni ya Kimataifa
By Michael Robinson BBC News
Nchi zinazoendelea zinachukua hatua kukabili ukwepaji kodi unaofanywa na makampuni makubwa ya kimataifa.
Zambia na Mongolia zimelieleza Shirika la Habari la BBC kuwa zinataka kuzuia utaratibu wa kampuni za uchimbaji madini kuhamisha faida yote kutoka kwenye nchi hizo kabla ya kutozwa kodi.
Nchi hizi mbili ni wazalishaji wakubwa wa madini na zinasema kwamba zinapoteza mabilioni ya dola kila mwaka ambazo nchi hizo zinahitaji kupitia kodi.
Hata hivyo, Shirika la Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo (OECD) limeonya kwamba hatua hizo zinaweza kuwa za hatari.
Shirika hilo la mataifa yaliyoendelea lenye makao yake jijini Paris, Ufaransa, linasema hatua za aina hiyo zinazofanywa na nchi moja moja zinaweza kusababisha mkanganyiko, sheria zisizoshikamana vema na kukosekana kwa viwango vinavyoeleweka vizuri.
Spika wa Bunge la Mongolia, Bw Z. Enkhbold, aliiambia BBC kwamba Mongolia ina mpango wa kufuta mikataba yote ya kimataifa ya mambo ya kodi ambayo makampuni ya uchimbaji madini yalikusudia kutumia ili kuhamisha faida kutoka nchini humo pasipo kulipa kodi ya uendeshaji.
“Kodi lazima ilipwe pale mahali inapoendeshwa biashara yenyewe halisi,” Bw Enkhbold aliiambia BBC, “na si katika nchi za ng’ambo”.
Athari itakuwaje
Sheria mpya nchini Zambia, ambayo itaanza kutumika mwezi huu, inataka makampuni yote ya uchimbaji madini kurejesha nchini humo ripoti kamili ya mauzo yanayofanyika. Baada ya ripoti hiyo kupelekwa Zambia, mamlaka ya mapato ya nchi hiyo itakagua gawio na malipo mengine ili kuona kama kuna uwiano halisi kabla ya faida hiyo kuhamishiwa nje ya Zambia.
“Hapa unazungumzia kuhusu wanawake wajawazito ambao hawana kliniki wanakoweza kwenda kwa ajili ya huduma za uzazi au elimu ya afya ya mtoto,” anasema Bw Guy Scott, Makamu wa Rais wa Zambia.
Makamu huyo wa Rais aliiambia BBC kwamba serikali yake inapoteza karibu dola bilioni 2 za Marekani kutokana na ukwepaji kodi ya uendeshaji kampuni.
“Tunazungumzia kiasi kikubwa sana cha fedha hapa,” alisema. Kiasi hicho ni kikubwa zaidi kuliko kile ambacho Zambia hutumia kila mwaka katika bajeti ya afya na elimu kwa pamoja.
“Unatazama watu ambao hawatapata elimu zaidi ya ngazi ya shule za msingi.”
Sheria mpya ya Zambia imeandaliwa katika namna inayohakikisha kuwepo kwa uwazi wa kimapato katika makampuni ya uchimbaji madini.
“Kwanza, hata hatujui akaunti hizo ziko wapi,” Bw Scott alieleza. “Walau sheria hii itafanya kuwa ni kosa la jinai kufanya ukwepaji wowote ule wa kulipa kodi. Inawalazimisha watu kuwa wawazi. Kwa sasa, wanakuwa wazi pale tu wao wenyewe wanapotaka kujitolea kuwa wazi.”
Chanzo: BBC News
Tafakari
Je, hali ya mambo iko vipi nchini Tanzania? Sekta ya madini ni miongoni mwa zinazochangia kwa kiasi kikubwa sana pato la nchi, lakini, je, kuna uwiano wa mapato kati kile kinachouzwa nje na kinacholipwa serikalini? Sheria zetu zinahakikisha uwazi katika mapato kwa kiwango gani? Je, tunajua wawekezaji hawa wakubwa akaunti zao ziko wapi? Tuna njia za kudhibiti kuhakikisha Taifa linapata gawio la haki na usawa? Je, mamlaka zenye dhamana ya kusimamia masuala haya zinatekeleza majukumu yao kikamilifu?
Tujenge nchi moja inayozingatia haki, usawa, amani, utengamao na unafuu wa kimaisha kwa kila mmoja huku kila mmoja akiwa na mazingira mazuri ya kutumia vipawa vyake kikamilifu kwa manufaaa yake mwenyewe na Taifa kwa ujumla. Tuna wajibu — kila mmoja wetu kuhakikisha tunafikia haya.
Fedha za Nje Zamwajibisha Waziri … Kashfa
Waziri wa zamani wa Fedha wa Ufaransa Jerome Cahuzac ajitoa kwenye kinyang’anyiro
Waziri wa Fedha aliyejiuzulu kwa kashfa wa Ufaransa Jerome Cahuzac — alikutwa na kashfa ya kuwa na fedha kwenye akaunti ambayo hakuiweka wazi kwenye benki moja nchini Uswisi — ametangaza kwamba hatagombea kiti chake katika uchaguzi mdogo.
Aliliambia gazeti la Depeche du Midi kuwa alihofia kukumbwa na kampeni chafu zenye vurugu.
Bw Cahuzac — ambaye hapo kabla alijizolea sifa kama msemaji hodari dhidi ya uwekaji kwa njia haramu wa fedha katika benki za kigeni — alijiuzulu mwezi Machi.
Kashfa hiyo ilizidi kuharibu sifa ya serikali ya Rais Francois Hollande ambayo tayari ilikuwa imeshachafuka.
Bw Cahuzac ametozwa faini kwa kosa la kutolipa kodi.
Mwanzoni alikana taarifa zilizotolewa na tovuti ya habari za uchunguzi kwamba alimiliki akaunti ambayo hakuiweka wazi katika benki moja nchini Uswisi hadi 2010.
Lakini baada ya kukutana na mahakimu wa uchunguzi mwezi Aprili, alikiri kuwa na akaunti hiyo ambayo ilikuwa na kiasi cha euro 600,000 (zaidi ya Shilingi bilioni 1.2).
Aliliambia gazei la Depeche kwamba tayari amekwishahamishia fedha hizo nchini Ufaransa na kwamba atalipa madeni yake kwa dola na kukabidhi kiasi kitakachobaki kwa taasisi za hisani.
Chanzo: BBC News
Mfalme Mpya … Tunajifunza Nini?
Willem-Alexander ameapishwa kuwa Mfalme wa Uholanzi kufuatia kujivua madaraka kwa Malkia Beatrix, mama yake.
Anakuwa mfalme wa kwanza tangu mwaka 1890. Mama yake, 75, alitia saini kukubali kwake kujivua madaraka aliyoyashikilia kwa miaka 33.
Umati mkubwa uliovalia mavazi yenye rangi ya machungwa ulitawala jiji la Amsterdam ili kushuhudia tukio hilo la kihistoria na kutoa heshima zao.
Mfalme mpya aliapa kuilinda katiba katika sherehe hizo zilizopambwa na kufana sana.”Ninaapa kulinda na kutunza uhuru na mipaka ya dola kwa nguvu zangu zote,” alisema Mfalme mpya.
“Nitalinda uhuru na haki za jumla na za kila mtu katika himaya yangu na nitatumia kila kilicho mikononi mwangu kwa mujibu wa sheria kuendeleza ustawi wa mtu mmojammoja na wa wote kama inavyostahili kufanywa na mfalme mwema … eeh Mungu unisaidie.”
Akiwa na umri wa miaka 46, mfalme huyu, ambaye mamlaka yake kisiasa yamepunguzwa sana, atalazimika kufanya kazi ya ziada ili kushawishi uwepo wa nafasi yake katika jamii.
Vijana wengi katika mitaa ya Amsterdam wanapata shida kuelewa lengo la kuwepo kwa familia ya kifalme — lakini wanapenda kusherehekea Siku ya Malkia.
Changamoto kubwa kwa Mfalme Willem-Alexander ni kuwaunganisha watu kwa ndani, kuwawakilisha kwa nje, na kuwajengea ari ya kufanya makubwa zaidi ili kuzidi kupanda juu.
Kwa upande wa mke wake, Maxima, ambaye sasa anakuwa malkia mpya, kuingia kwake kwenye ukoo wa kifalme wa Uholanzi kulikuwa na msisimko mkubwa.
Akiwa ni mzaliwa wa Amerika ya Kusini, familia yake ilichunguzwa kuona kama ilikuwa na uhusiano wowote na utawala wa kidikteta ulipata kutawala nchi yake ya asili — Argentina. Hata hivi, uchangamfu wake ulilichangamsha taifa.
Binti huyu wa ukoo wa kifalme alijitosa kwenye maji ya baridi na kuogelea huko Amsterdam: ilikuwa ni utayari wake wa kuyakabili maji hayo ya baridi sana ili kukusanya fedha za hisani kuwa jambo lililowavuta wengi miongoni mwa raia wa Kidachi.
“Amekuja na ameshinda,” anasema mwanahistoria wa Kidachi Henk te Velde.
“Ni muhimu aonyeshe kwamba anatambua nafasi yake — kuwa pembeni mwa mfalme na si malkia mkuu”, anasema mwanahistoria Han van Bree. Anaongeza kusema kwamba utayari wake kuzungumza na watu katika lugha yao baada ya kuolewa na Mwana mfalme Willem-Alexander, lilikuwa jambo lililopokelewa vema.
“Watu walivutiwa na ukweli kwamba mara baada ya kufika hapa, alianza mara moja kujifunza Kidachi,” anasema te Velder. “Tulivutiwa naye. Alionyesha kwamba anatuheshimu na anafanya jitihada kutuelewa”.
“Sasa hivi, ana uwezo hata wa kutaniana kwa Kidachi.”
Chanzo: BBC News
TUNAJIFUZA NINI?
- Wenzetu wanadumisha utamaduni wao, kitu kinachowaunganisha na kuwafanya wamoja kwa lengo la kuleta maendeleo ya wote.
- Kuna umuhimu wa kuheshimu misingi yetu ya asili inayotuunganisha, kutusaidia kuheshimu utu wa mtu, kutusaidia kusukuma maendeleo yetu sote, kutusaidia kukua zaidi kama binadamu, kuenzi na kuheshimu uhuru wa mtu mmojammoja kuwa vile wanavyotaka kuwa ili mradi hawavunji sheria, na misingi inayotusaidia kufikiri kwa usahihi na kisayansi
- Kutunza lugha zetu za asili na kuwafundisha wengine. Hii inahusu sana pia Lugha ya Kiswahili, tukienzi, tukitunze na tukieneze kwa jamii nyingine
- Tujifunze historia yetu ili kutusaidia kujua tunatoka wapi, wapi tulifanya makosa, tuyasahihishe vipi, na tufanye nini ili kufika kule tunakotaka kwenda
- Bila shaka nawe umejifunza mengi … unaweza kutushirikisha. Karibu.
Dar … Ongeza Majina ya Vitongoji
Naam. Dar es Salaam ina vitongoji vingi. Kuna vile vilivyo maarufu kwa sababu ni vya miaka mingi, vingine kwa sababu ya aina ya watu wanaoishi huko, huku vingine vikiwa kwa sababu ya sifa na matukio yanayotokea huko. Hata hivyo, kuna vitongoji vingine ambavyo vinachipukia siku hizi … kwa kiasi kikubwa ni makazi mapya. Kadiri muda utakavyoruhusu tutakuwa tukivitembelea na kupata taswira chache.
Tuanze na Kitongoji cha Mwanagati. Barabara kuu ya kukufikisha Mwanagati ni ile inayoingilia Banana, kupitia Kipunguni na Kitunda. Alama kubwa ni Shule ya Sekondari Mzinga. Huko kuna eneo lililopimwa chini ya Mradi wa Viwanja 20,000. Kuna makazi yanayokuja juu kwa kasi na tayari kuna huduma nyingi muhimu.
Pia kuna barabara inayotokea Tandika. Hii lakini bado sijaipita.
Kwa ujumla mandhari hapa ni tambarare, udongo unaotawala ni kichanga. Kuna barabara za mitaa zilizowekwa wakati wa upimaji, na maji yanapatikana kwa kudrill ardhi wastani wa mita 60. Maji yanayopatikana ni baridi. Ni eneo ambalo nyakati za jioni, kuna mkondo wa upepo unaopita na bila shaka kwa wale wanaopenda utulivu … mbali na kelele za magari, huku watapapenda.
Hapo juu ni taswira chache zinazoonyesha mitaa ya kitongoji hicho.
Pamoja sana.























